Lugha, Mawasiliano na Mizozo: Mikakati ya Mawasiliano katika Kesi za Mizozo kwenye Mahakama ya Juu ya Mazingira na Ardhi ya Jiji la Kisumu
Keywords:
Lugha, mahakama, mikakati ya mawasiliano, mizozo, ujihusishajiAbstract
SWAHILI
Makala hii inalenga kuchunguza mikakati ya mawasiliano inayotumika katika kesi za migogoro ya umiliki wa ardhi katika Mahakama ya Juu ya Mazingira na Ardhi ya Jiji la Kisumu. Utafiti uliongozwa na Nadharia ya Ujihusishaji iliyoasisiwa na Giles (1973) na kuendelezwa na Giles et al. (1991). Nadharia hii inaeleza kuwa washiriki katika mawasiliano hubadilisha matumizi yao ya lugha kulingana na muktadha, utambulisho na malengo ya mazungumzo. Data ilikusanywa nyanjani kwenye Mahakama ya Juu ya Mazingira na Ardhi ya Jiji la Kisumu. Kundi lengwa lilikuwa mawasiliano ya kesi sita ambazo zilikuwa zimeratibiwa kusikizwa katika mahakama hiyo mwezi wa Oktoba 2019. Usampulishaji wa dhamira ulitumiwa kuteua Mahakama ya Juu pamoja na kesi nne ambazo ziliendeshwa kwa lugha ya Kiswahili. Mbinu ya uchunguzi usio wa kushiriki ulitumika kukusanya data. Baada ya data kukusanywa, ilipangwa na kuchanganuliwa kupitia mbinu ya uhakiki wa yaliyomo. Matokeo yamewasilishwa kwa njia ya maelezo. Matokeo ya utafiti yanaonyesha kuwa mawakili, hakimu, walalamishi na washtakiwa hutumia mikakati mbalimbali ya mawasiliano ambayo inaweza kuibua migogoro ya kimawasiliano au kuimarisha maelewano kati ya washiriki. Mikakati hii huwa na athari kubwa katika ufanisi wa mchakato wa maamuzi ya kesi. Makala hii inaonyesha kuwa lugha hutumiwa kama chombo muhimu cha utatuzi wa migogoro, lakini matumizi yake yanategemea sana mikakati ya mawasiliano yanayochaguliwa na washiriki. Makala hii inapendekeza kuwa, mahakama ihimize kutumiwa kwa mikakati ya mawasiliano ambayo itachochea athari chanya katika mawasiliano licha ya tofauti za kimamlaka baina ya wazungumzaji. Aidha, watafiti wa baadaye wachunguze mikakati ya mawasilano inayotumika kupitia njia ya kidijitali kwa kuwa hivi karibuni, vikao vya mahakama vinaendeshwa kupitia mitandao.
ENGLISH
Keywords: Communication strategies, conflicts, courts, engagement, language
Downloads
Published
How to Cite
Issue
Section
Copyright (c) 2025 Samuel Sinzore Ogonda, Eddah Martha Njeri

This work is licensed under a Creative Commons Attribution-NonCommercial-ShareAlike 4.0 International License.

